Ikiwa imebaki siku moja kabla miamba miwili ya soka ya
Manchester haijakutana Jumatatu tarehe
30 April 2012, joto na hamasa za wachezaji, mashabiki, watazamaji na wadau
wote zinazidi kupanda.
Manchester Derby ni jina linalotambulisha mchezo
unaozikutanisha timu mbili zinazotoka Manchester yaani Manchester City wanaotoka mashariki mwa Manchester wenye maskani
yao Etihad Stadium na Manchester United wanaotoka Trafford
wenye maskani yao Old Trafford
Manchester City FC
Timu hizi zimekuwa na rekodi ya mahudhurio makubwa zaidi
ya watazamaji katika mechi zao za nyumbani. Tiketi kwa ajili ya kuingia
uwanjani Etihad Stadium tarehe 30 Aprli 2012 zilikuwa zimekwisha (zimeuzwa zote) zaidi ya wiki mbili kabla ya pambano.
Mechi ya mwisho kati ya timu hizi mbili ambayo ni ya 162 baina yao, ilikuwa kwenye mzunguko
wa tatu wa Kombe la FA, Januari 8, 2012
Etihad Stadium ambapo Manchester
United iliondoka na ushindi wa magoli 3 – 2. Mechi inayofuata itakuwa
Jumatatu tarehe 30 April 2012 kwenye uwanja huo huo wa Etihad.
UMUHIMU WA MECHI HII KWA TIMU ZOTE
Katika msimamo wa ligi hivi
sasa, timu ya Manchester United iko
mbele ya Manchester City kwa pointi
tatu (3) huku timu zote zikiwa zimecheza michezo 35. Hivyo basi kuna uwezekano
wa Manchester City kuongoza ligi endapo itaifunga Manchester United Jumatatu.
Upepo ulianza kugeuka taratibu
pale Manchester United walipokutana
na Wigan Athletic tarehe 11 April 2012 kwenye uwanja wa DW stadium na kupata kipigo cha goli 1 – 0 huku wapinzani wao Manchester City wakiwashushia kipigo cha
magoli 4 – 0 West Brom siku hiyo hiyo. Ushindi huu wa Manchester City ulianza kupunguza tofauti ya pointi baina yake
na Manchester United kutoka nane hadi tano; hali kadhalika kujiongezea akiba ya magoli ya kufunga ambayo pia imekuwa silaha ya
timu hii pale inapotokea kufunga kwa pointi na mshindani wake.
Yule Bundi mweusi aliendelea
kukaa kwenye paa ya nyumba ya Manchester
United pale walipokutana Timu ya Everton
katika uwanja wa Old Traford Jumapili
tarehe 22 Aprili 2012 na kulazimishwa sare
ya magoli 4 – 4 huku wapinzani wao Manchester
City wakiifunga the Wolves mabao 2 –
0 na kuishusha daraja. Matokeo haya ya Jumapili yalizidi kutia Nuru kwenye
jitihada za Manchester City kunyakua Ubingwa wa EPL huku yakipeleka wasiwasi
mkubwa kwa wapinzani wao wa Old traford kwani tofauti ya Pointi sasa ilikuwa ni Pointi 3
Hakuna shaka kuwa matokeo na
muendelezo huo katika ligi hasa kwa vigogo hivi viwili vya Manchester unaufanya
mpambano wa Jumatatu 30, Aprili 2012 kuwa
mpambano muhimu sana kwa kila timu na kuongeza hamasa kwa wadau kushuhudia
pambano hilo.
Kati ya mwaka 1992 mpaka 2011
kumekua na mashindano 19 ya ubingwa wa ligi ya premier ambapo Manchester United
imefanikiwa kuchukua ubingwa huo mara 12. Kwa takwimu hizo ni Manchester United
ambayo imechukua ubingwa mara nyingi zaidi kuliko klabu nyingine yoyote,
ubingwa wa mwisho ukiwa ule aliouchuku msimu wa 2010/11. Mashabiki na wapenzi
wa Manchester united hawangependa kupoteza historia na muendelezo huo wa
ubingwa.
Kwa misimu miwili mfululizo,
Manchester City imewekeza katika kununua wachezaji mahiri katika harakati zake
za kujiimarisha na kunyakua ubingwa ambao hawajawahi kuutwaa na hivyo ni
mategemeo ya mashabiki wake kulinyakua kombe hilo mwaka huu. Manchester City
wasingependa kuona jitihada hizi zikienda bure hasa katika kipindi hiki ambacho
matumaini ya ushindi yamerudi tena baada ya kupotea pale April 8 2012. Mashabilki,
wapenzi na wadau wote wangependa kuona kwa mara ya kwanza ubingwa unabaki
Etihad. Mchezaji mahiri na kocha wa Zamani wa Manchester City, Kevin Keagan
anaamini kuwa ushindi wa katika mechi yake na Manchester United Jumatatu,
itaihakikishia timu hiyo Ubingwa msimu huu na kulibakiza kombe Etihad.
Makocha wa timu zote mbili
wanajua umuhimu wa mechi hii huku Kocha wa Manchester United Sir Alex Fergusson
akisema kuwa mechi hii ndio muhimu zaidi katika miaka yake yote 26 katika
uongozi wa soka ....“Ni mchezo muhimu ambao utaamua bingwa , tuna nafasi nzuri
zaidi kuliko Man City. Wenyewe wanahitajika kushinda, sisi tunaweza kutoka sare
au kushinda. Tutajitahidi kushinda”
Manchester City haijafanikiwa
kushinda katika mechi zake tatu za kombe la Premier zilizochezwa uwanja wa nyumbani
Etihad lakini itakuwa ikijiamini kutokana na ushindi wake wa magoli 6 – 1 dhidi
ya Manchester United Mwezi October 2011.
Kocha wa Manchester
City Roberto Mancini anaona kuwa Manchester United bado wana nafasi kubwa ya
kuchukua ubingwa wa Premier Ligi pamoja na ukweli kwamba kuna tofauti ya pointi
tatu tu baina ya timu hizo mbili. Mancini alisema kuwa “Ni muhimu kushinda
katika mchezo huu, kiwango si muhimu sana , tumecheza vizuri katika msimu mzima
lakini cha muhimu kwa sasa ni Kushinda”
Baada ya hekaheka
za Champions league zilizohusisha miamba ya Hispania Barcelona na Real Madrid;
Macho na masikio ya wapenzi wengi wa soka yako Etihad Jumatatu tarehe 30 Aprili
2012





No comments:
Post a Comment